Mwanamke aliyejulikana kwa jina
la Doroth Msuya, mkazi wa Monduli mkoani Arusha, ametoweka muda mfupi kabla ya
kufunga ndoa na Joseph Machange, mkazi wa Mwika, Wilaya ya Moshi mkoani
Kilimanjaro.
Ndoa ya wawili hao ilitarajiwa kufungwa Jumamosi ya Novemba 7
katika Kanisa la Kinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) Dayosisi ya
Kaskazini, Usharika wa Lole, Mwika.
Mchungaji mwenza wa usharika huo, Elikeseni Shao, alisema majira
ya saa sita na nusu mchana wakati maandalizi ya ibada ya ndoa yakiwa
yamekamilika, walipokea taarifa za kutoweka kwa bibi harusi huyo akiwa saluni.
“Sisi kama viongozi wa kanisa tulipokea kwa masikitiko taarifa
za kutoweka kwa aliyekuwa bibi harusi mtarajiwa wakati akiwa saluni, na kwamba
liliwashtua sana ikizingatiwa kuwa maandalizi yote ya ndoa yalikwisha kamilika
na kumuacha bwana harusi solemba,” alisema.
Alisema uongozi wa kanisa hilo baada ya kupewa
taarifa hizo iliwalazimu kuitisha kikao cha familia zote mbili na kuzungumza
nao juu ya tukio hilo ambapo pia walichukua hatua ya kuzifanyia maombi familia
hizo ili zisiingie katika mawazo ya imani za kishirikina.
Akielezea mazingira ya tukio hilo, mmiliki wa saluni aliyokuwa
akipambiwa bibi harusi, Stella Mringo, alisema awali alimpokea mteja huyo saa
nne asubuhi na ilipofika saa sita na nusu mchana alimuomba amruhusu atoke
kwenda kujisaidia.
Alisema bibi harusi huyo alitoka nje akiwa na mpambe wa watoto
aliyefahamika kwa jina moja la Esther.
“Lakini mpambe huyo alirudi na kuchukua khanga ya bibi harusi na
alipotoka tena hakumkuta,” alisema.
Kwa upande wake, mshereheshaji wa sherehe hiyo, William Ngalo,
alisema akiwa kwenye ukumbi wa sherehe uitwao Mamba Complex, alipokea
taarifa kuwa asiendelee na kazi ya kufunga muziki kwa kuwa kuna matatizo
yamejitokeza, na alipofuatilia alijulishwa kuwa bibi harusi alitoweka katika
mazingira ya kutatanisha.
Alisema bibi harusi huyo alitafutwa eneo lote la Mwika
bila kupatikana jambo lililolazimu chakula kilichoandaliwa katika sherehe hiyo
kuliwa nyumbani kwa wazazi wa bwana harusi majira ya saa tatu usiku.
Kwa upande wake, baba wa bwana harusi mtarajiwa, Eliringia
Machange, alisema wao kama familia wamepokea kwa masikitiko tukio hilo na kwa
sasa hawawezi kusema chochote.
Bwana harusi mtarajiwa, Joseph Machange, alisema jambo
lililomtokea haliamini kwani limemuumiza, hasa baada ya kutumia fedha zaidi ya
milioni saba kwa ajili ya maandalizi ya harusi hiyo.
Alisema kwa sasa suala hilo limeripotiwa katika kituo kidogo cha
polisi Himo, na kwamba wanasubiri uchunguzi uendelee.
No comments: