Rais John Magufuli anatarajiwa, wakati wowote kuanzia sasa,
kuwateua baadhi ya watu wenye sifa kuwa wabunge ili aweze kuwapa majukumu ya
kuongoza wizara atakapopanga safu ya Baraza la Mawaziri, hivi karibuni.
Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 inampa
Rais mamlaka ya kuteua wabunge wasiozidi 10 kutoka miongoni mwa wananchi ambao
anaona wanaweza kumsaidia katika utekelezaji wa majukumu yake katika baadhi ya
maeneo kama vile afya, elimu, kilimo, nishati na sheria.
Ibara ya 66 (1) inasema, bila ya kuathiri masharti mengine ya
ibara hii, kutakuwa na aina zifuatazo za wabunge, yaani (e) wabunge wasiozidi
10 walioteuliwa na Rais kutoka miongoni mwa watu wenye sifa kwa mujibu wa ibara
ya 67, isipokuwa sifa iliyotajwa katika ibara ya 67(1) (b).
Baraza hilo jipya linatarajiwa kuwa na sura nyingi mpya ambazo
zitaendana na kasi yake kutekeleza kaulimbiu ya “Hapa Kazi Tu.” Pia, baraza litakuwa
na sura mpya kutokana na ukweli kwamba baadhi ya mawaziri waliangushwa kwenye
kura za maoni, wengine wakati wa Uchaguzi Mkuu na wengine, japokuwa wamerejea
bungeni ni walionekana kuwa mzigo awamu iliyopita.
Kati ya mawaziri 55 waliokuwamo katika Baraza lililopita,
waliorejea katika Bunge la 11 ni 23 tu wakiwamo 20 wa majimbo na watatu wa viti
maalumu. Kupungua kwa idadi hiyo kutampa Dk Magufuli fursa ya kusuka baraza
hilo kutoka miongoni mwa wabunge 188 wa majimbo, 64 wa viti maalumu na 10
atakaowateua ili wamsaidie.
Haijulikani baraza litakuwa na mawaziri wangapi ila wakati wa
kampeni amewahi kukaririwa akisema litakuwa dogo ikilinganishwa na lililopita.
Katika muhula wa pili wa utawala wake, Rais Kikwete aliwateua
wabunge 10, kati yao sita aliwapa wizara za kuongoza, utaratibu ambao huenda Dk
Magufuli akautumia ili kupata mawaziri kulingana na mahitaji ya Serikali
atakayoiunda.
Kwanza Rais Kikwete alimteua Profesa Makame Mbarawa na akamfanya
Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia; na Shamsi Vuai Nahodha ambaye
alipewa Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa. Pia, alimteua Zakhia Meghji
lakini hakumpa wizara, na Mwenyekiti wa NCCR-Mageuzi, James Mbatia (sasa mbunge
mteule wa Vunjo).
Baada ya kufanya mabadiliko ya Baraza la Mawaziri mwaka 2012,
Rais Kikwete aliwateua Profesa Sospeter Muhongo (sasa mbunge mteule wa Butiama)
akampa Wizara ya Nishati na Madini; Janet Mbene na Saada Salum Mkuya akawafanya
manaibu waziri katika Wizara ya Fedha.
Janet ambaye baadaye aliteuliwa kuwa Naibu Waziri wa Viwanda na
Biashara ameshinda ubunge katika Jimbo la Ileje na Mkuya anasubiri hatima yake
katika Jimbo la Kijitoupele, Zanzibar. Aidha, alimteua Dk Asha-Rose Migiro kuwa
Waziri wa Katiba na Sheria na hivi karibuni alikamilisha orodha kwa kuwateua Dk
Grace Puja na Innocent Sebba.
Baraza la Mawaziri litajulikana baada ya wabunge kula kiapo wiki
ijayo mbele ya Spika wa Bunge ambaye anatarajiwa pia kuchaguliwa wiki ijayo.
No comments: